
Jumapili ya leo tarehe 16/07/2023 imekuwa siku ya furaha na baraka tele kwa familia ya Baba Askofu Dkt. Msafiri Joseph Mbilu ambaye akiambatana na familia yake, wamemtolea Mungu sadaka ya shukrani kwa namna Mungu alivyomtetea Binti yao Sarah hasa wakati wa Ugonjwa wa CORONA.

Katika Ibada iliyofanyika Kanisa Kuu Lushoto,ikiongozwa na Baba Askofu Jacob Ole Moreto Paulo Mameo wa KKKT-Dayosisi ya Morogoro. Askofu Dkt. Mbilu amesema kuwa yeye na familia yake wanawiwa kumshukuru Mungu kwa jinsi alivyomlinda Binti yao Sarah katika kipindi chake cha Masomo cha miaka 6 nchini China. "Lililokubwa kwetu kama Familia ni kuona jinsi Mungu alivyomtetea Binti yetu hasa wakati wa Ugonjwa mbaya wa CORONA ambao ulianzia pale Wuhan kwenye Chuo ambacho alikuwa anasoma binti yetu.
Wakati wa CORONA tulijaribu kumuondoa Sarah arudi nyumbani lakini tulishindwa kabisa. Pale tuliposhindwa tulinyoosha mikono na kumuachia Mungu, leo mioyo yetu imejaa furaha kubwa tunapoona Sarah amemaliza masomo yake ya Shahada ya kwanza ya Utabibu (Bachelor of Medicine) na kurejea nyumbani salama. Katika furaha hii tumeona tumtolee Mungu Shukrani ya pekee" Amesema Askofu Dkt. Mbilu.

Sadaka iliyopatikana katika Ibada hiyo ya Shukrani ilikuwa fedha taslim Milioni nne na elfu sita (Tsh. 4,006,000), ahadi Milioni tatu na laki nane (Tsh. 3,800,000/=) na kufanya jumla kuu kuwa shilingi Milioni Saba laki nane na elfu sita (7,806,000). Kiaisi hiki kilicho patikana kimeelekezwa kulipia deni kubwa la Dayosisi.Askofu Dkt. Msafiri Mbilu amewashukuru ndugu jamaa na marafiki waliofanikisha kupatika kwa kiasi hicho kitakacho saidia katika ulipaji wa Deni la Dayosisi.
