Print

Askofu wa KKKT-Dayosisi ya Kaskazini Mashariki, Mch Dkt. Msafiri Joseph Mbilu amesema anaimani na wakurugenzi wapya waliochaguliwa hivi karibuni kusimamia Kurugenzi mbalimbali za Dayosisi huku akiwataka waumini pamoja na wakuu wa vituo vya Dayosisi kuwapa ushirikiano ili waweze kutimiza malengo yanayokusudiwa.



Askofu Dkt. Mbilu, ameyasema hayo katika Ibada ya Jumapili ya tarehe 12/05/2024 iliyofanyika katika Jimbo la Tambarare Usharika wa Korogwe na kuongeza kuwa sasa Kurugenzi zote za Dayosisi zimekamilika kwakuwa na Wakurugenzi wenye sifa baada ya nafasi hizo kukaimiwa kwa kipindi kirefu, hivyo anaamini Wakurugenzi hao utendaji wao wa kazi utaleta matokeo chanya na manufaa kwa Dayosisi.

Wakurugenzi hao wapya ni Mkurugenzi wa Uchumi, Mipango na Maendeleo Bibi, Pendo Wilfred Lauwo na Mkurugenzi wa huduma za jamii Bw. Afizai Vuliva. Aidha Baba Askofu amemtambulisha Rasmi Mkuu wa Jimbo Mteule wa Jimbo la Tambarare Mch. John Ndimbo na hivyo kumtakia baraka za Mungu katika utendaji wake wa kazi huku akimtaka kuendeleza mambo mazuri aliyoyafanya mtangulizi wake Mch. Frank Mtangi. Mch. John Ndimbo amechukuwa nafasi ya kuliongoza Jimbo la Tambarare baada ya Mtangulizi wake Mch. Frank Mtangi kuhamishiwa Jimbo la Pwani.

Ibada hii iliyoambatana na matendo mbalimbali pia Washarika wa Usharika wa Korogwe waliitumia Ibada hiyo kuungana na Wanadayosisi kwa ujumla kumuombea na kumtakia heri na baraka Baba Askofu Dkt. Mbilu, kufuatia kufikisha miaka Mitatu (3) toka kuingizwa kazini.

Ikumbukwe kuwa Baba Askofu Dkt. Msafiri Joseph Mbilu, aliingizwa kazini katika Ibada iliyofanyika Kanisa Kuu Lushoto tarehe 09/05/2021, na kisha yeye kumuingiza kazini msaidizi wake, Mch. Michael Mlondakweli Kanju hivyo 09/05/2024 alitimiza miaka hiyo mitatu ya kuiongoza KKKT-Dayosisi ya Kaskazini Mashariki.