Mei 9 mwaka 2021 ilikuwa ni siku iliyotawaliwa na nderemo, vifijo na shamrashamra katika viunga vya Lushoto, siri nyuma ya furaha hii si nyingine bali ni historia mpya kuandikwa, wakristo wa KKKT-Dayosisi ya Kaskazini Mashariki walipata Askofu mpya, kiongozi ambae atayabeba maono na dira ya KKKT-Dayosisi ya Kaskazini Mashariki huyu sio mwingine bali ni Askofu Dkt. Msafiri Joseph Mbilu.

Baba Askofu Dkt. Mbilu, aliingizwa kazini katika Ibada iliyofanyika Kanisa Kuu Lushoto tarehe 09/05/2021, na kisha yeye kumuingiza kazini msaidizi wake, Mch. Michael Mlondakweli Kanju. sasa leo tarehe 09/05/2024 ni miaka mitatu ya Uongozi wa Baba Askofu Dkt. Msafiri Joseph Mbilu tangu alipopewa kibali na Mungu cha kuiongoza KKKT-Dayosisi ya Kaskazini Mashariki.
 
Leo tarehe 09/05/2024 zimetimia siku 1,096, yaani miaka mitatu tangu alipoingizwa kazini kushika wadhifa huo , bado tunaiona shauku ileile ndani yake kwani licha ya kusimamia mafundisho sahihi ya Neno la , Askofu Dkt. Mbilu amesimamia msingi wa Dayosisi katika kumhudumia mwanadamu kimwili, kiakili na kiroho.

Askofu Dkt. Mbilu licha ya kusimamia Dayosisi kupitia kauli mbiu yake ya kasi tofauti, ameendelea kuwa mnyenyekevu na msikivu kwa washarika wote  kwani anaamini ushirikiano mzuri wanaompa ndio msingi wa mafaniko ya Dayosisi.

 
Askofu Dkt. Msafiri Joseph Mbilu, pamoja na msaidizi wake Mch. Michael Kanju, wameshiriki kwenye uchaguzi wa kumpata Askofu Mpya wa Sinodi rafiki ya Southeastern Pennsylvania, iliyoko Philadelphia nchini Marekani , ambapo uchaguzi huo uliofanyika leo tarehe 05/05/2024 umekamilika na Mch. Bryan Penman amechaguliwa kuwa Askofu Mteule akichukuwa nafasi ya mtangulizi wake
 Askofu Dkt. Patricia Davenport aliyemaliza muda wake.

Katika uchaguzi huo Askofu Mteule Mch. Penman amepata ushindi dhidi ya mshindani wake wa karibu Mch. Karl Richard.

Askofu wa KKKT-Dayosisi ya Kaskazini Mashariki, Mch Dkt. Msafiri Joseph Mbilu, anaendela na ziara yake ya kikazi iliyoanza tarehe 26/04/2024 nchini Marekani katika Mji wa Philadelphia, ambako ndiko Makao Makuu ya Synod rafiki ya Southeastern Pennsylvania yalipo. Hii ni mojawapo ya Synod za Kanisa la Kiinjili la Kilutheri Marekani.

Mchungaji Jeremia Mboko wa KKKT-Dayosisi ya Kaskazini Mashariki, Jimbo la Pwani Usharika wa Mikanjuni amewashukuru na kuwapongeza waumini wa Usharika huo ambao wanaendelea kujitoa katika kuchangia deni linalo ikabili Dayosisi huku akiwataka washarika wote kuingia kazini kikamilifu katika kuchangia deni hilo.