Uncategorised
- Details

Mkuu wa Kanisa la Kiinjili la Kilutheri Tanzania Askofu Dkt. Fredick Onael Shoo amewaasa wanafunzi wa Shule ya Sekondari Lwandai inayomilikiwa na KKKT-Dayosisi ya Kaskazini Mashariki kusoma kwa bidii na kumtanguliza Mungu katika masomo yao ili kutimiza ndoto zao.

Ameyasema hayo leo tarehe 01/08/2022 akihitimisha ziara yake ya siku 6 ndani ya KKKT-Dayosisi ya Kaskazini Mashariki katika Jimbo la Kaskazini wakati wa ufunguzi wa maabara ya kujifunzia masomo kwa vitendo ambayo imefanyiwa ukarabati mkubwa katika Shule ya Sekondari Lwandai, huku akifurahishwa na matokea mazuri na kuahidi kuwa balozi wa Shule hiyo.

Askofu Dkt. Shoo pia ameupongeza uongozi wa Dayosisi chini ya Askofu Dkt. Joseph Mbilu, kwa jitihada mbalimbali zilizofanywa na uongozi kwa kuanza kurudisha uhai katika Shule hiyo hivyo kuwa na matumaini kuwa shule hiyo itakuwa ni moja ya Shule bora kitaifa.


Kwa upande wake Askofu wa KKKT-Dayosisi ya Kaskazini Mashariki Dkt Msafiri Joseph Mbilu amesema kuwa Mlalo ndio kitovu cha Dayosisi na kusisitiza kuwa wapo watumishi mbalimbali ambao wamezaliwa na wengine kutumika katika Usharika wa Mlalo sambamba na kusema kuwa Shule ya Lwandai imekuwa na historia kubwa kwakuwa ndipo ilipoanzia Shule ya Sekondari Eliboru na Chuo kikuu cha Makumira.

Nae Mbunge wa Jimbo la Mlalo Mhe. Rashidi Shangazi ameahidi kushirikiana na Kanisa katika mambo mbalimbali yanayohitaji msaada kutoka serikalini ili kupata msaada wa haraka sambamba na kushukuru Kanisa kwa kutoa huduma muhimu kwa jamii ikiwemo mashule Hospitali na vituo vya huduma ambavyo kipekee vinamilikiwa na Kanisa.

Ikumbukwe kuwa ziara ya mkuu wa Kanisa la Kiinjili la Kiluther Tanzania katika Dayosisi ya Kaskazini Mashariki ilianza tarehe 27/7/2022 na kuhitimishwa tarehe 01/08/2022 ambapo katika ziara hiyo ametembelea sharika na vituo mbalimbali vya huduma pamoja na kuweka mawe ya msingi katika Sharika za Dayosisi. Hapo kesho Mkuu wa KKKT atapata nafasi ya kuagana na mwenyeji wake Askofu Dkt. Msafiri Joseph Mbilu ndipo atakapo rejea katika majukumu yake.



- Details

Mkuu wa Kanisa la Kiinjili la Kilutheri Tanzania Askofu Dkt. Fedrick O. Shoo ameshuhudia kuwa, kwa huduma mbalimbali za kijamii zinazoendelea kutolewa na KKKT-Dayosisi ya Kaskazini Mashariki ni ishara nzuri inayodhihirisha nafasi yake kama Kanisa katika kufanya huduma za Diakonia ndani ya jamii.

Mkuu huyo wa KKKT ambaye pia ni mwenyekiti wa Jumuiya ya Kikristo Tanzania (CCT) amesema kuwa katika vituo mbalimbali alivyotembelea wakati wa ziara yake inayoendelea KKKT-Dayosisi ya Kaskazini Mashariki amekuta watoa huduma wenye furaha na kazi wanayoitenda hali inayodhihirisha kuwa wanayo matumaini licha ya changamoto zinazoikabili Dayosisi.

Askofu Dkt. Shoo amebainisha hayo leo 31/7/2022 wakati akitoa salamu zake kwenye Ibada ya siku ya Bwana ya saba baada ya Utatu aliyoiongoza akiwa kwenye Usharika wa Kanisa Kuu Lushoto.

Mbali na hayo amepongeza ushirikiano mzuri uliopo baina ya viongozi wa KKKT-Dayosisi ya Kaskazini Mashariki na Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ambao umejidhihirisha kwa vitendo wakati wote wa ziara yake.

Awali Mkuu wa Wilaya ya Lushoto ambae pia ni Mwenyekiti wa Kamati ya Ulinzi na Usalama Wilaya Mhe. Kalisti Lazaro amesema kuwa Serikali na Kanisa wamekuwa wakishirikiana katika maendeleo kwa muda mrefu na kipekee Dayosisi ya Kaskazini Mashariki imekuwa ikitekeleza wajibu huo kwa kupeleka huduma mbalimbali za maendeleo katika maeneo ambayo wakati mwingine serikali haikufika.

Katika hatua nyingine Askofu wa KKKT-Dayosisi ya Kaskazini Mashariki Dkt. Msafiri Joseph Mbilu alimueleza Mkuu wa Kanisa kuwa wanadayosisi ya Kaskazini Mashariki wanajisikia fahari kuwa sehemu ya kazi za umoja wa Kanisa na miongoni mwa wanajumuiya ya Kikristo Tanzania (CCT) hivyo imekuwa ikitoa na kuwasilisha michango yote inayopaswa kufanya hivyo.


- Details

Mkuu wa Kanisa la Kiinjili la Kilutheri Tanzania Askofu Dkt. Fredrick O. Shoo amewataka Wakristo kuwa mstari wa mbele katika kushiriki katika zoezi la sensa ya watu na makazi inayotarajiwa kufanyika Nchini Agosti 23 mwaka huu na kuwahimiza Wachungaji na Mashemasi kuendelea kuwakumbusha waumini mara kwa mara kujiandaa na zoezi hilo.
Askofu Dkt. Shoo ambaye pia ni Mwenyekiti wa Jumuiya ya Kikristo Tanzania (CCT) amesema kuwa zoezi hilo litasaidia kuweza kupata idadi sahihi ya wananchi itakayo isaidia serikali katika mipango yake mbalimbali ya sasa naya baadae.

Mkuu wa KKKT ameyasema hayo leo tarehe 30/07/2022 wakati akitoa salamu zake kabla ya Mahubiri kwenye Ibada ya kuwabariki vijana wa Kipaimara 21 miongoni mwao wawili walibatizwa iliyofanyika Usharika wa Makorora, Jimbo la Pwani ambako anaendelea na ziara yake rasmi ya kikazi.

Pamoja na hayo Askofu Dkt. Shoo amelikumbusha Kanisa kuendelea kuiombea nchi kama lifanyavyo katika sala kuu kila Ibada ya Jumapili, kuombea uongozi wake na Rais Samia Suluhu Hassan i ili Mungu aendelee kuwajaza hekima, afya njema, ujasiri, moyo wa huruma na upendo.Amesema viongozi wakipata baraka hizo nchi itabarikiwa, haki na mshikamano utaendelea kuwepo kwa watu wote.

Awali Kabla ya Ibada Mkuu wa Kanisa aliweka jiwe la msingi la Kanisa hilo la Makorora ambapo kwa upande wake Askofu wa KKKT- Dayosisi ya Kaskazini Mashariki, Dkt. Msafiri Joseph Mbilu amewashukuru wote waliojitolea kukamilisha ujenzi huo akiwemo Waziri wa Nishati ambae pia ni Mbunge wa Bumbuli Mhe. Januari Makamba.

Mara baada ya Ibada hii msafara wa Mkuu wa KKKT umerejea Wilayani Lushoto yalipo Makao Makuu ya KKKT-DKMs ambapo kesho tarehe 31/07/022 Askofu Dkt. Shoo majira ya asubuhi ataongoza Ibada ya jumapili katika Usharika wa Kanisa Kuu Lushoto na baadae mchana atatembelea vituo vya Irente Rainbow School, Irente Children’s Home, Irente School for the Blind na Irente Farm.


Mkuu wa Kanisa atahitimisha ziara yake siku ya tarehe 01/08/2022 katika Jimbo la Kaskazini (Mlalo) ambapo pia kutafanyika Ibada katika Usharika wa Mlalo na majira ya mchana ataelekea katika Shule ya Sekondari Lwandai ambapo Baba Askofu Dkt. Shoo atafungua Jengo la Maabara ambalo lilifanyiwa ukarabati mkubwa na majira ya jioni msafara wa Mkuu wa Kanisa utaelekea katika Chuo Kikuu kitarajiwa cha Kolowa Technical Training Institute (KOTETI).


- Details
Mkuu wa Kanisa la Kiinjili la Kilutheri Tanzania (KKKT) Askofu Dkt. Fredrick O. Shoo ameelezea kufurahishwa kwake na waumini wa KKKT-Dayosisi ya Kaskazini Mashariki kwajinsi walivyotambua umoja wa Kanisa ulivyo na nguvu katika kufanikisha kazi ya Mungu.
Mkuu huyo wa KKKT Askofu Dkt. Shoo ameeleza hayo leo tarehe 29/07/2022 akiwa katika Ibada ya Shukrani iliyofanyika kwenye Jimbo la Tambarare Usharika wa Korogwe ikiwa ni mwendelezo wa ziara yake KKKT-Dayosisi ya Kaskazini Mashabiki.
Askofu Dkt. Shoo amesema inapendeza kuona jinsi mioyo ya wanadayosisi ya Kaskazini Mashabiki ilivyo imarika na kuheshimu umoja wa Kanisa kwa kujitoa kushiriki katika kazi mbalimbali.
Katika hatua nyingine Askofu Dkt. Shoo amewataka wanadayosisi ya Kaskazini Mashabiki kuendelee kuwaombea muda wote viongizi wa Dayosisi ili waendelee kuitenda vyema kazi ya Mungu bila kuchoka.
Pamoja na hayo Mkuu wa KKKT hakusita kumshukuru Askofu Dkt. Joseph Mbilu kwa kazi za diakonia ndani ya Dayosisi na kuongeza kuwa KKKT-DKMs imekuwa mfano katika Kanisa kwa kuwaendea wenye shida maalamu wanao hitaji msaada kwani huo ndio utambulisho wa Kanisa la KKKT.
Askofu Dkt. Shoo leo ametembelea Usharika wa Korogwe, Usharika wa Muheza na akiwasili katika Jimbo la Pwani ameanza ziara yake katika Usharika wa Pongwe na baadae aliwasili yalipo Makao Makuu ya Jimbo la Pwani Usharika wa Kana. Hapo kesho Askofu Dkt. Shoo anatazamiwa kuweka jiwe la Msingi la Kanisa Katika Usharika wa Makorora na kuongoza Ibada ya Kipaimara katika Usharika huo.
Page 75 of 124

